Yona 2 (NEN)
Maombi ya Yona na kuokolewa
1Akiwa ndani ya tumbo la samaki, Yona alimwomba Bwana Mungu wake. 2Akasema:
“Katika shida yangu nalimwita Bwana,
naye akanijibu.
Kutoka kina cha kaburi2:2 Kaburi hapa maana yake ni Kuzimu; kwa Kiebrania ni Sheol. niliomba msaada,
nawe ukasikiliza kilio changu.
3 Ulinitupa kwenye kilindi,
ndani kabisa ya moyo wa bahari,
mikondo ya maji ilinizunguka;
mawimbi yako yote na viwimbi
vilipita juu yangu.
4 Nikasema, ‘Nimefukuziwa
mbali na uso wako,
hata hivyo nitatazama tena
kuelekea Hekalu lako takatifu.’
5 Maji yaliyonimeza yalinitisha,
kilindi kilinizunguka;
mwani ulijisokota kichwani pangu.
6 Nilizama chini sana hata pande za mwisho za milima,
makomeo ya hiyo nchi yalinifungia hata milele.
Lakini uliuleta uhai wangu kutoka shimoni,
Ee Bwana Mungu wangu.
7 “Uhai wangu ulipokuwa unatoka,
nilikukumbuka wewe, Bwana,
nayo maombi yangu yalikufikia wewe,
katika Hekalu lako takatifu.
8 “Wale watu wanaoshikilia sanamu batili
hupoteza neema yao.
9 Lakini mimi nitakutolea dhabihu,
kwa sauti za shukrani na shangwe.
Lile nililowekea nadhiri nitalitimiza.
Wokovu watoka kwa Bwana.”
10 Basi Bwana akamwamuru yule samaki, naye akamtapika Yona katika nchi kavu.