Zaburi 120 (NEN)

Zaburi 120
Kuomba msaada dhidi ya wadanganyifu
Wimbo wa kwenda juu.
1 Katika dhiki yangu namwita Bwana,
naye hunijibu.
2 Ee Bwana, uniokoe kutoka midomo ya uongo
na ndimi za udanganyifu.
3Atakufanyia nini,
au akufanyie nini zaidi, ewe ulimi mdanganyifu?
4 Atakuadhibu kwa mishale mikali ya shujaa,
kwa makaa yanayowaka ya mti wa mretemu.
5 Ole wangu kwa kuwa naishi Mesheki,
kwamba naishi katikati ya mahema ya Kedari!
6Nimeishi muda mrefu mno
miongoni mwa wale wanaochukia amani.
7Mimi ni mtu wa amani;
lakini ninaposema, wao wanataka vita.