Zaburi 127 (NEN)
Zaburi 127
Bila Mungu, kazi ya mwanadamu haifai
Wimbo wa kwenda juu. Wa Sulemani.
1 Bwana asipoijenga nyumba,
wajengao hufanya kazi bure.
Bwana asipoulinda mji,
walinzi wakesha bure.
2 Mnajisumbua bure kuamka mapema
na kuchelewa kulala,
mkitaabikia chakula:
kwa maana yeye huwapa usingizi wapendwa wake.
3 Watoto ni urithi unaotoka kwa Bwana,
uzao ni zawadi kutoka kwake.
4 Kama mishale mikononi mwa shujaa
ndivyo walivyo wana awazaao mtu katika ujana wake.
5 Heri mtu ambaye podo lake
limejazwa nao.
Hawataaibishwa wanaposhindana
na adui zao langoni.